NAMNA YA KUKUZA NA KUIMARISHA ROHO YAKO- 5
Baada ya kuangalia kwa undani
kuhusu neno la Mungu, kusifu na kuabudu na jinsi kunavyoweza kuimarisha roho
yako, ni wakati mzuri sasa kujifunza namna maombi yanavyoweza kuikuza na kuimarisha
roho yako. Kama nilivyotangulia kusema, namna hizi zote zinalenga katika
kumkaribia Mungu (kuwa karibu na Mungu). Kwa hiyo njia hizi ukizitumia ipasavyo
zitakufanya umkaribia Mungu zaidi hatua kwa hatua. Ukaribu huu ndio unaofanya
mahusiano kati ya Mungu na mtu kuimarika. Ili kuelewe jambo la maombi namna
linavyoweza kuimarisha na kukuza roho yako, ni vizuri kukueleza kidogo maana ya
maombi.
Maana ya maombi
Maombi yanatazamwa kwa mtazamo
tofauti kwenye biblia. Maombi kwa jinsi ya mwili yanajulikana kama kuhitaji
msaada juu ya mahitaji ambayo mtu anayo. Kitu ambacho ni sawa lakini tuangalie
biblia inasemaje. Kibiblia maombi yana mitazamo tofauti lakini yote ikimlenga
Mungu:-
a.
Maombi
ni mawasiliano baina ya Mungu na mwanadamu
b.
Maombi
ni ushirika (fellowship) kati ya mtu na Mungu
c.
Maombi
ni njia ya kuwasilisha na kupokea mahitaji yetu kwa Mungu
Kwa somo hili tutachukua tafsiri
ya kwamba maombi kama ushirika kati ya mtu na Mungu kwa sababu tukienda kwa
picha hii na pia tukifanya hivi (fellowship na Mungu) ndipo tunaweza kujenga
roho zetu na kuziimarisha.
Inapofika wakati kujenga na
kuimarisha roho yako, inapaswa kutanua fikra kuona maombi zaidi ya kuona ni
njia ya kupeleka mahitaji yetu kwa Mungu, bali kuona ni sehemu ya ushirika na
Mungu. Na Mungu anataka tuone ni sehemu ya ushirika kati yetu na yeye kuliko kama
njia tu ya kupeleka mahitaji ingawa mahitaji yetu tunaweza kuyapokea tu kwa
maombi pekee.
Namna ya kupokea mahitaji
Biblia iko wazi kwamba kwa maombi
pekee tunaweza kupokea mahitaji yetu kutoka kwa Mungu hii ni kutokana na jinsi
Mungu alivyotengeneza mfumo wake wa namna ya kumsaidia mwanadamu. Kwa hiyo mtu
asipoomba asitegemee kitu toka kwa Mungu. Yakobo 4:2 anatuambia:- “…..wala
hamna kitu kwa kuwa hamwombi”. Ni muhimu sana kujua kwamba vitu kutoka kwa
Mungu tunaweza kuvipata kwa njia ya maombi. Kwa hiyo tunaweza kuongeza vitu
kutoka kwa Mungu maisha mwetu kwa njia ya maombi. Yeye aliye mvivu kuomba,
ndivyo na vitu vya Mungu vitakuwa adimu maishani mwake.
“Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni nanyi mtaona; bisheni, nanyi
mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona, naye
abishaye hufunguliwa” Math 7:7-8
Biblia inatuhakikishia kwamba
ombeni nanyi mtapewa, na kila aombaye hupokea. Ona hapa, Mungu anatoa wito wa
kuomba juu ya mahitaji yetu, na sentensi hii inatuonesha kwamba tunachokiitaji
kipo stoo, ukiomba unapewa. Mungu anamwambia kila mmoja kuwa ukiomba utapewa
unachokiomba. Lakini yeye achukuaye hatua ya kuomba, sio kwamba atapewa yeye hupokea.
Wakati anaomba ulikuwa sio wakati wa kusema atapewa lakini ni wakati wa
kupokea. Kwa hiyo maombi ni njia ya kupokea mahitaji yetu kwa Mungu. Maombi sio
tu kwamba tunapeleka mahitaji bali tunapokea mahitaji yetu kutoka mwa Mungu.
Kwa sababu kila aombaye hupokea. Hii ni kutokana kwamba tunatakiwa kuomba kwa
imani.
“Kwa sababu hiyo nawaambia, yoyote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba
mnayapokea, nayo yatakuwa yenu” Marko 11:24
Omeona hapo? Tunayapokea
tunayoyaomba wakati wa kuomba. Hili ni jambo la muhimu kulifahamu. Wengi baada
ya kuomba ndiyo wanajiandaa kupokea, biblia haisemi hivyo, inasema “maana kila
aombaye, hupokea…” kupokea ni kwa kila anayeomba kama akiomba sawa sana na
mapenzi ya Mungu. Kwa njia ya maombi tunapokea tunayoyahitaji, kwa hiyo hakuna
maombi hakuna mahitaji. Huo ndio mpango wa Mungu.
Katika kujenga mausianao yetu na
Mungu ni vizuri kuona maombi kwa sura nyingine kabisa. Sio tu kwamba maombi ni
njia ya kupokea mahitaji yetu bali pia ni sehemu ya ushirika na Mungu. Maombi yanapokuwa
kama ushirika kati ya Mungu na mwanadamu, mambo mawili hutokea kwa haraka; moja,
mtu ataenda kwenye maombi sio kwa sababu ana mahitaji tu na pili, huyo mtu
haitamsumbua hata asipopata analichokuwa anakiomba kwa sababu gafla uhusiano
wake na Mungu unakuwa haujengwi katika mahitaji anayoyaomba bali katika upendo
na ushirika dhabiti. Kuona maombi kama njia ya kujenga na kuimarisha ushirika
na Mungu ni bora zaidi kuliko kuona maombi kama njia ya kupokea mahitaji yetu
kwa sababu, kigezo kimojawapo kinachomfanya Mungu kukupa unachokiomba ni
mahusiano (ushirika) mazuri kati yako na yeye. Kwa kadiri unapoendelea kujenga
ushirika naye ndivyo na hofu (kumcha) yake inavyozidi kujengeka ndani yako.
“Yeye,
siku hizo za mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika
mauti,maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, na akasikilizwa kwa
ALIVYOKUWA MCHA MUNGU”
Waebrania 5:7
Mstari huu unazungumza kwa habari
ya Yesu Kristo alipokuwa katika mwili. Alimtolea Mungu maombi na dua pamoja na
kulia na machozi, lakini alisikilizwa na kujibiwa sio kwa sababu tu aliomba na
kulia na machozi bali kwa sababu alikuwa mcha (hofu ya) Mungu. Maombi, dua na
machozi yana nafasi yake, lakini wakati mwingine kama uhusiano wako na Mungu
sio mzuri kuna mambo huwezi kupata. Mungu anaweza kusikia maombi yako na
kuyaona machozi yako na kukujibu kama mfalme Hezekia (2 Wafalme 20:5).
Ni vizuri mtu akalenga katika
kuimarisha mahusiano yake na Mungu katika maombi ili kuhakikisha kwamba kila
analoliomba analipokea. Ili kufanikisha kujenga mahusiano na Mungu ni vizuri
kukumbuka mambo kadhaa, la kwanza, Mungu ni Roho kwa hiyo unaweza kuwasiliana
naye kwa roho yako, la pili, maombi hufanyika rohoni (moyoni) yaani mtu anapaswa
kuomba kwa moyo wake wote iwe akili zake zina matunda ama hazina matunda.
Kutengwa na uso wa Mungu
Wakati wa maombi ni wakati wa
kuonekana mbele za Mungu kabisa na kuzungumza naye, yaani roho yako inakutana
na Roho ya Mungu katika maombi. Niweke wazi kwamba mara baada ya Adamu kufanya
dhambi ilitutenga na uso wa Mungu.
“Walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya
usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” Mwanzo 2:17
Mungu alimtahadharisha Adamu
kwamba usile hayo matunda na siku utakapokula hakika utakufa, neno “utakufa”
lilikuwa halimaanishi kufa kwa jinsi ya mwili bali kwa jinsi ya rohoni yaani
kutengwa na uso wa Mungu.gafla macho ya Adamu ya rohoni yakafungwa yasiweze
kuona mambo ya Mungu na macho ya mwilini kufunguka. Akawa mbali na Mungu kwa
sababu ya dhambi, makosa na uovu juu ya Mungu. Ushirika na ukaribu wa Mungu kwa
Adamu ukawa hakuna tena, Adamu alikuwa hawezi kuzungumza na Mungu kama mwanzo
ilivyokuwa.
“Lakini
maovu yenu yemewafarakanisha ninyi Na Mungu wenu, dhambi zenu zimeuficha USO
wake msiuone, hata hataki kusikia”
Isaya 59:2
“Acheni
kuniletea sadaka zisizokuwa na maana! Uvumba wenu ni chukizo kwangu. Miandamo
ya Mwezi, Sabato na mikutano ya ibada, siwezi kuvumilia makusanyiko yenu maovu.
Sikukuu zenu za Miandamo ya Mwezi na sikukuu zenu zilizoamriwa moyo wangu
unazichukia. Zimekuwa mzigo kwangu, nimechoka kuzivumilia. Mnaponyosha mikono
yenu katika kuomba, nitaficha macho yangu nisiwaone, hata mkiomba maombi mengi
sitasikiliza. Mikono yenu imejaa damu”
Isaya 1:13-15
Madhara ya makubwa ya dhambi ni
kututenga na Mungu, hata tusiweze kuuona uso wake. Maana dhambi zinatuficha
mbali na uso wa Mungu. Adamu kukimbilia sehemu ya kujifisha ilikuwa ndicho
kilichotokea na alichokuwa anajisikia rohoni kwa wakati ule. Ile kukimbia
ilikuwa ni ishara ya kitu kilichotoa rohoni mwake. Ndio maana hata sasa
ukifanya dhambi hasikii ndani yako kukaa karibu na Mungu na unajisikia kukaa
mbali. Kwa sababu mtu hujisikia kuhukumiwa kila wakati. Hata kama alikuwa
anafanya kwa siri, gafla utakuta haunekani alipokuwa anapatikana siku zote,
mahali pa maombi, kusifu na kuabudi, kusoma neno n.k. Hii ni kwa sababu kila
akiomba, haoni akijibiwa, akiinua mikono yake, Mungu anauficha uso wake.
Lakini Mungu alichokikusudia
tangu mwanzo tunakiona pia katika Zekaria 3:7 anapotuambia;
“BWANA wamajeshi asema hivi, kama ukienda katika njia zangu na kama
ukishika maagizo yangu, ndipo utakapoihukumu nyumba yangu, nawe utazilinda nyua
zangu, nami nitakupa nafasi ya KUNIKARIBIA kati yao wasimamao karibu”
Nijaribu mfano huu, kuna wakati
wanandoa wanaweza wakawa hawaishi nyumba moja kutokana na majukumu ambayo kila
moja anakuwa nayo (safari za kikazi, au kuhama kikazi) ingawa ni hakika
wanatakiwa kukaa nyumba moja tena chumba kimoja zaidi sana kitanda kimoja.
Katika hali hizi zote mbili, wanatakiwa kuwa karibu sana kimahusiano kwa sababu
wameshakuwa mwili mmoja. Ingawa Mungu anahitaji mahusiano ya karibu sana na
wanadamu lakini pia anakuhitaji mahali alipo karibu sana naye, madhabahuni, mbele
ya kiti cha enzi mbinguni. Kusudia la Mungu ni kwamba mwanadamu awe anakaribia
mbele za kiti chake cha enzi wakati wote, ndiyo maana hapo anamwambia Yoshua
kuhani kwamba kama ukifuata maagizo na njia zangu (akiachana na dhambi na uovu),
nitakupa nafasi ya kukaribia mbele zake. Anaposema “nitakupa nafasi”
inatuonyesha wazi kwamba kuna “nafasi” ya wanadamu mbele za kiti cha enzi
iliyowekwa na Mungu ambayo dhambi imeifanya hiyo nafasi kuwa wazi kwa sababu
wanadamu wakawa hawezi tena kukaribia hapo.
MAHALI PATAKATIFU
Katika harakati za kurudisha kile
ambacho Adamu alikipoteza hatimaye na wote waliozaliwa naye kupoteza (nafasi ya
kukaribia mbele za Mungu), Mungu anaamua kumwambia Musa kujenga hema sawa sawa
na alivyomunesha katika mlima. Hii hema ilikuwa ni picha ya mahali patakatifu
pa mbinguni. Akamwambia hivi;-
“Simamisha
Hema sawasawa na ramani uliyoonyeshwa kule juu mlimani, Tengeneza pazia la
nyuzi za buluu, za zambarau na za rangi nyekundu na kitani safi iliyosokotwa
vizuri, fundi stadi atarizi makerubi kwenye hayo mapazia. Litundike kwa kulabu
za dhahabu kwenye nguzo nne za mti wa mshita ambazo zimefunikwa kwa dhahabu,
zikiwa zimesimamishwa kwenye vitako vinne vya fedha. Ning’iniza pazia hilo
kwenye vifungo, kisha weka sanduku la Ushuhuda nyuma ya pazia. Pazia
litatenganisha Patakatifu na Patakatifu pa Patakatifu. Weka kifuniko cha kiti
cha rehema juu ya sanduku la Ushuhuda ndani ya Mahali Patakatifu pa Patakatifu”
Kutoka 26:30-34
Hema hiyo ilikuwa na sehemu kuu
tatu, sehemu ya kusanyiko la Israeli, patakatifu na Patakatifu pa Patakatifu.
Patakatifu pa Patakatifu palikuwa panatengwa na Patakatifu kwa pazia. Hapo
palikuwa panahudhuriwa na kuhani mkuu tu. Ilikuwa ndiyo sehemu ya ndani kabisa
ya hema, sanduku la ushuhuda (agano), na kiti cha rehemu juu ya hilo sanduku.
Na makerubi yaliyokuwa yanafunika kiti cha rehema kwa mbawa zao. Ndipo palipoitwa mahali patakatifu na pa kukutania. Hapo mahali ndipo Mungu
alipokuwa amemwambia Musa atakuwa akisema naye.
“Saga baadhi yake
kuwa unga na uweke mbele ya sanduku la Ushuhuda ndani ya Hema la Kukutania,
mahali ambapo NITAKUTANA nawe. Itakuwa takatifu sana kwenu” Kutoka 30:36
“Kwa vizazi vijavyo itakuwa kawaida kutoa sadaka hii ya kuteketezwa kila
mara kwenye ingilio la Hema la Kukutania mbele ya BWANA. Hapo ndipo
NITAKAPOKUTANA na ninyi na KUSEMA nanyi, Huko ndipo nitakapokutana na
Waisraeli, nalo Hema la Kukutania litatakaswa na utukufu wangu” Kutoka
29:42-43
“Weka hiyo madhabahu
mbele ya lile pazia lililo mbele ya Sanduku la Ushuhuda lililo mbele ya kiti
cha rehema kilicho juu ya Sanduku la Ushuhuda, mahali ambapo nitakutana nawe” Kutoka 30:6
Katika mistari hii yote, ni vyema
kuona kwama mahali patakatifu palikuwa na madhabahu, sanduku la ushuhuda na
kiti cha rehema kilichowekwa juu ya sanduku la ushuhuda, hapo ndipo Mungu
alipokuwa anakutana nao na kusema nao. Kutokea kwenye mistari hii tunaona mambo
mawili ya haraka. La kwanza, sio mahali popote pa hema ya kukutania Mungu
alikuwa akisema bali kutokea sehemu ya patakatifu pa patakatifu palipokuwa na
kiti cha rehema, la pili wale ambao walikuwa hawa nafasi ya kupaingia
patakatifu yaani kusanyiko la Israeli walikuwa wanasubiri kuhani aliyekuwa na
hiyo nafasi aje awaambiye alichosema Mungu. Kusanyiko lote la Israeli lilikuwa
halina nafasi ya kukaribia patakatifu pa patakatifu kwa sababu ya pazia.
Watu wengi pia tunaishi maisha
haya kama kusanyiko la Israeli, hawataki kuomba, wanasubiri waombewe na
kuletewa majibu na wengine. Na maisha yao yanakuwa tofauti na wale wanaoingia
pale patakatifu pa patakatifu. Kila wakati ambao Musa alikuwa anataka kuongea
na Mungu alikuwa akienda ndani ya pazia mbele ya kiti cha rehema, na Mungu
alikuwa akisema naye kutokea hapa. Musa alijua huo ndio utaratibu ambao Mungu
amejiwekea kuwasiliana na mimi baada ya kusimamisha hema ya kukutania. Musa
alifanyia maombi yake hapo, kwenye hiyo madhabahu na mbele ya kiti cha rehema
baada ya kupita kusanyiko la Israeli na patakatifu. Nilitaka uone mahali ambapo
akina Musa walikuwa wanatolea maombi yao na kuzungumza na Mungu. Mungu
alitamani kuzungumza nao akiwa karibu.
Barikiwa na endelea kufatilia mwendelezo wa somo hili, karibia tunafika mwisho.
NAMNA YA KUKUZA NA KUIMARISHA ROHO YAKO- 5
Reviewed by Unknown
on
10:44:00 AM
Rating:

Amen
ReplyDeleteasant tumejifunza