NEEMA YA MUNGU INAVYOWEZA KUKUSAIDIA KUSHINDA MAJARIBU NA KUISHI MAISHA YA USHINDI KATIKA ULIMWENGU HUU

Utangulizi
Fahamu Aina ya Ulimwengu Tunaoishi
Ulimwengu
huu tunaoishi ni ulimwengu wa shida, adha, mateso, majaribu, uliojaa uovu,
dhambi na machafu ya kila aina, biblia inautaja kama “…….dunia hii mbovu
iliyopo sasa…..” (Galatia 1:4). Kila kukicha asubuhi, ukigeuka huku na huku, ukisafiri
huku na kule, utasikia na kuona ukishuhudia maasi, maovu yanayoendelea
ulimwenguni humu, hakika ni mambo ya kutisha. Dunia hii imejaa katika kukosa na
kumkana BWANA na katika kugeuka isimtafute Mungu, ikinena jeuri na uasi na
kukusudia maneno ya uongo na kuyatoa moyoni, hukumu imegeka ikaenda nyuma na
haki inasimama mbali sana, maana kweli imeanguka katika njia kuu na kupungua kabisa
na unyofu hauwezi kuingia. Licha ya haya
yote yanayoendelea, ndio ulimwengu tunaoishi kwa sasa, na bado Mungu anahitaji
tuishi maisha ya ushindi ya kumpendeza.
Hii
iko wazi kabisa kwamba shetani ndio chanzo au kwa maneno mengine kwake ndiko
yalikoanzia lakini mwanadamu ndiye aliyeruhusu yakapata nafasi na nguvu juu
yake mwenyewe na ulimwengu mzima. Kwa mfano biblia inatuarifu kwamba “Ninyi ni
wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye
alikuwa muuaji tangu mwanzo, wala hakusima katika kweli kwa kuwa hamna hiyo
kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe kwa sababu yeye ni
mwongo na baba wa huo” (Yoh 8:44). Hii inatuonesha kwamba Ibilisi ndiye chanzo
au mwanzilishi wa uongo na uuaji na ndani yake kumejaa huo na mbegu yake
uiachilia ndani yao wote wanaoambatana naye. Neno baba maana yake chanzo au
mwanzilishi na mmiliki. Mungu ni baba yetu kwa sababu wanadamu wote tuliumbwa
kutoka kwake, tunaowaita baba kwa jinsi ya mwili ni kwa sababu tumetokea kwao
kwa jinsi ya mwili ndio maana wanasayansi wanasema kibiologia mtoto ni wa baba na sio wa mama kwa sababu mtoto
hatokei kwa mama bali hutokea kwa baba ndio maana hata vinasaba (DNA) vinapimwa
kwa baba.
Kwa
mantiki hiyo shetani ndiye mwanzilishi wa uongo, uuaji na adha nyingine, na
anapofanikiwa kupata umiliki wa watu anapandikiza ile mbegu na hao watu
hujikuta kutamani kufanya yaliyo mapenzi ya baba yao au mmiliki wao ambaye ni
shetani.
Kama
nilivyotangulia kusema hapo mwanzo,
ingawaje shetani ambaye ndiye Ibilisi ndiye chanzo au mwanzilishi wa
machafu, maovu, adha, dhambi na maasi, shida na majaribu yote tunayoyajua na
tusiyoyajua lakini mwanadamu ndiye aliyeyafungulia mlango na kuyarusu
ulimwenguni kufanya kazi na kuwa na nguvu juu yake mwenyewe.
Biblia inasema
“Kwa hiyo, kama kwa mtu mmoja dhambi
iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti, na hivyo mauti ikawafikia
watu wote kwa sababu watu wote wamefanya dhambi” (Rum 5:12)
Kwa hiyo yote tuyaonayo yaliyo kinyume na
mapenzi ya Mungu yaliingia ulimwenguni kupitia kwa mtu mmoja aliyeyaruhusu
kuingia. Neno ’iliingia’ linaonesha wazi kwamba dhambi ilitumia mlango uliokuwa
tayari kuiruhusu kupita, ikiwa na maana kwamba dhambi haikukutana na kikwazo
chochote mlangoni ambacho kingeweza kuzuia kwa hiyo vikwazo viliondolewa na
mlinda mlango na kuuacha mlango kuwa wazi na dhambi ikaingia. Ni vizuri kujua
hili kwamba wakati wote dhambi iko mlangoni inasubiri kuingia katika ulimwengu
wako na kuleta madhara. Mungu alimwambia Kaini “……dhambi iko, inakuotea
mlangoni, nayo inakutamani wewe….” Mwa 4:7
Tukisoma
katika Mwanzo 1:26-28 tunaona wazi kwamba Mungu aliyeumba mbingu na nchi na
vyote vilivyomo ndani yake alimpa mwanadamu aliyemuumba kumiliki na kuitawala
nchi na vyote vilivyomo ndani yake kama mfalme. Utawala na umiliki huo ulikuwa
unalenga uitiisha nchi, bahari na vyote vilivyo ndani yake kwa taratibu na
sheria za mbinguni ambazo kwa wazi zingeonesha uhalisia wa tabia na matendo ya Mungu duniani. Dunia itawaliwe na tabia na
matendo ya Mungu ikiwa ni pamoja na upendo na utakatifu na kufanya ulimwengu
kuwa mahali sahihi pa kuishi na kustawi. Mungu alikusudia matunda ya mbegu yake
yawe ndiyo pekee yanayofahamika na kujulikana ulimwenguni kote, ili kutimiza
hazma hii aliiumba sura(tabia) yake ndani ya mwanadamu kabla ya kumpa ufalme
ili huyo mwanadamu atakapotawala azae matunda ya sura hiyo.
Lakini
tunaona wazi anguko lake lilivyokuwa kubwa kwa huyo mwanadamu baada ya
kushindwa kushika na kutii maagizo ya Mungu. Anguko hilo ilibadilisha umiliki
wa ulimwengu kutoka kwa mwanadamu kwenda kwa shetani na shetani kuitwa mungu au
mkuu wa ulimwengu huu (Yoh 14:30), lakini pia wakati Yesu anajaribiwa, shetani
“….akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu na
fahari yake, akamwambia haya yote nitakupa, ukinisujudia” (Math 4:8-9),
inaonesha wazi kwamba shetani alipata umiliki wa ulimwengu na fahari yake yote
kwa sababu asingesema nitakupa kama sio yeye mmiliki lakini pia Yesu hakubishia
umiliki huo wa shetani alichokataa ni kusujudia.
Baada
ya shetani kupata umiliki wa ulimwengu na fahari yake yote, kazi yake ilikuwa
moja tu, kuujaza ulimwengu kwa tabia zake na matendo yake. Maovu, machafu,
dhambi na mabaya ya kila namna na alifanikiwa kwa kiasi kikubwa. Mfano fikiri
pamoja nami wakati wa Nuhu jinsi ambavyo aliweza kuijaza tabia yake ndani ya
watu wote wa ulimwengu akapona mtu mmoja tu (Nuhu). Ulimwengu mzima uliambatana
na kutenda tamaa za baba yao Ibilisi.
Ni
vizuri kuelewa kwa kina aina ya ulimwengu tunayoishi. Shetani baada ya kupata
nafasi ya kumiliki huu ulimwengu alifanikiwa kutengeneza mfumo wake ambao watu
wanaishi kwa huo na kudumisha utamaduni wake. Watu wakilala na kuamka wako
kwenye huo mfumo na utamaduni, kila kizazi kinachotokea ulimwenguni kinazaliwa
na kukulia katika huo mfumo na utamaduni ambao unadhibiti na kuratibu mwenendo
wa maisha yao na kuamua aina ya maisha yao.
Utamaduni
ni kama “vacuum” iliyooandaliwa tayari ambacho watu
huzaliwa na kukua ndani yake. Kwa hiyo shetani alitengeneza vacuum/ utamaduni
wa ulimwengu ambao watu watazaliwa na kukulia ndani yake. Watu wote tukazaliwa
na kukulia katika ulimwengu ulio na mfumo na utamaduni wa maovu, mabaya,
makosa, madhambi, magonjwa, adha, shida za kila aina na machafu yote
tukayakubali na kuyapa kipaumbele kama yaliyo ya thamani kwetu. Kitu chochote
kinabadilika kuwa utamaduni kama kitaonekana na kitakubaliwa na watu wa jamii
na kufanywa kuwa sehemu ya maisha katika shughuri za kila siku. Ndivyo ilivyokuwa
na ndivyo ilivyo ulimwenguni humu.
Biblia inazungumza habari za Lutu na wale
wageni wawili waliomtembelea kwamba “hata kabla hawajalala, watu wa mji,
wenyeji wa Sodoma, wakaizunguka nyumba, vijana
kwa wazee watu wote waliotoka pande zote. Wakamwambia Lutu, wa wapi wale
watu waliokuja kwako usiku huu? Uwatoe kwetu tupate kuwajua” (Mwa 19:4-5). Watu
wote wa mji wa Sodoma walizaliwa na kukua katika utamaduni wa uzinzi. Kwao
waliona ni jambo jema, wakalikubali na kuona ni sehemu ya maisha yao. Watoto
walizaliwa na kukulia katika vacuum ya uzinzi na kuona ni jambo la kawaida
kwao. Kwa mfano pia kipindi tulichonacho sasa, imezoeleka kwamba kijana ambaye
hajafikia umri wa kuoa au kuolewa haiwezekani akaishi bila kuwa na mpenzi wa
jinsia nyingine. Ni utamaduni sasa kwamba kijana ni lazima awe na mpenzi wake
hata kama bado hajafikia umri wa kuoa au kuolewa. Watoto wanazaliwa na kukukua
katika kawaida hiyo, wakiona ni jambo jema nao wanaliendeleza. Ni hafadhari ya
nchi za Afrika, lakini nchi za ulaya na nchi za magharibi ni ukweli mtupu
katika jambo hili.
Endelea
kufatilia mwendelezo wa Somo Hili
NEEMA YA MUNGU INAVYOWEZA KUKUSAIDIA KUSHINDA MAJARIBU NA KUISHI MAISHA YA USHINDI KATIKA ULIMWENGU HUU
Reviewed by Unknown
on
5:47:00 PM
Rating:

No comments: